Ads 468x60px

Blogroll

Blogger news

About

mafundisho

Tunaendelea tena leo, kujifunza Kitabu cha YOHANA katika Biblia zetu. Leo tunatafakari YOHANA 7:17-52. Ingawa kichwa cha somo letu la leo ni, “JINSI YA KULIELEWA NENO LA MUNGU“, kuna mengi zaidi ya kujifunza katika mistari hii. Tutayagawa mafundisho yote tunayoyapata katika mistari hii, katika vipengele kumi:-



(1) JINSI YA KULIELEWA NENO LA MUNGU (MST. 17);

(2) JINSI YA KUMTAMBUA NABII WA KWELI (MST. 18);

(3) KUSHINDWA KWA WANADAMU WOTE KUISHIKA TORATI (MST. 19);

(4) SABABU KUU YA KUMWITA MTUMISHI WA MUNGU KWAMBA ANA PEPO (MST. 19-20);

(5) WAJIBU NA JINSI YA KUHUKUMU (MST. 21-24);

(6) SABABU KUU YA WATU WENGI KUSHINDWA KUMPENDA MUNGU (MST. 25-29);

(7) SAA YA KUKAMATWA (MST. 30);

(8) NAMI NILIPO NINYI HAMWEZI KUJA (MST. 33-36);

(9) MITO YA MAJI YALIYO HAI (MST. 37-44);

(10) KOSA LA KUMHUKUMU MTU KABLA YA KUMSIKIA (MST. 31-32, 45-

52).


(1) JINSI YA KULIELEWA NENO (MST. 17)

Biblia, ni kitabu kinachochapishwa na kutolewa nakala nyingi sana na kusambazwa na kusomwa kwa wingi, kuliko Kitabu chochote kile kingine ulimwenguni, katika wakati wote na miaka yote. Kwa mfano, kulingana na vitabu vyenye takwimu, “ENCYCLOPAEDIA BRITANNICA“ na “ENCYCLOPAEDIA AMERICAN“, mwaka 1932 peke yake Biblia zilizoschapishwa na kusambazwa kwa lugha mbalimbali duniani, zilikuwa 1,330,213,815. Miaka 50 iliyopita kulingana na mtafiti anayeitwa HY PICKERING, ili kukidhi mahitaji ya Biblia, Chama cha Biblia cha BRITISH AND FOREIGN BIBLE SOCIETY, kililazimika kuchapa nakala moja ya Biblia kila baada ya SEKUNDE TATU mchana na usiku au karibu nakala 32,876 kila siku katika mwaka mzima. Biblia hizi zilisambazwa katika ulimwengu mzima kwa kutumia makasha 4,583 yenye uzito wa karibu TANI 500! Hata hivyo, jambo la kushangaza ni kwamba mamilioni ya watu wanaosoma Biblia hawaielewi! Tunajuaje kwamba hawaielewi? Maisha ya watu hawa hayabadiliki na kufuata maelekezo ya Neno la Mungu. Tatizo ni nini? Jibu tunalipata katika MST. 17 “MTU AKIPENDA KUYATENDA MAPENZI YAKE (MUNGU), ATAJUA HABARI YA YALE MAFUNZO“. Kama mtu hayuko tayari kulitenda kila jambo atakalofundishwa na Mungu katika Neno lake, Roho Mtakatifu humwacha mtu huyo, hawezi kumfunulia chochote katika Neno la Mungu. Matokeo yake hawezi kuelewa lolote! Bila roho Mtakatifu hatuwezi kufunuliwa na kulielewa Neno la Mungu (1 WAKORINTHO 2:10, 13; YOHANA 16:13). Wengi wetu hatulielewi Neno kwa sababu hatuko tayari kulitendas. Hatua yoyote ya kushindana na kupingana na Neno la Mungu, humfanya Roho Mtakatifu kutuacha mara moja. Kabla ya kulisoma neno au kujifunza Neno la Mungu kwa njia yoyote, ili tulielewe Neno la Mungu, hatuna budi kuwa na msimamo wa kutaka kulitenda Neno lake sawasawa na (YEREMIA 42:1-6).



(2) JINSI YA KUMTAMBUA NABII WA KWELI (MST. 18)

Yeye anenaye kwa nafsi yake tu, huyo siyo nabii wa kweli. Kunena kwa nafsi yake mtu, ni kuhubiri au kufundisha kinyume na Neno la Mungu. Mtu wa jinsi hii, hatafuti Utukufu wa Mungu, bali wake mwenyewe. Nabii wa kweli humhubiri Kristo, au kwa jinsi nyingine, hulihubiri Neno! (WAFILIPI 1:18; 2 TIMOTHEO 4:2).



(3) KUSHINDWA KWA WANADAMU WOTE KUISHIKA TORATI (MST. 19)

Wanadamu wote mble za macho ya Mungu, hakuna hata mmoja aliyeweza kuishika torati, maana mtu akiishika sheria yote, ila akajikwaa katika neno moja, anahesabiwa kukosa juu ya yote (YAKOBO 2:10). Hivyo, mbele za Mungu, hakuna mwanadamu atendaye mema, la, hata MMOJA! (WARUMI 3:10, 12; 1 YOHANA 1:8). Wanadamu wote tulistahili kuangikwa msalabani kama adhabu ya laana ya kutokuishika torati (WAGALATIA 3:10; KUMBUKUMBU 21:22-23). Aliyempendeza Mungu sikuzote, na kufanya yaliyompendeza, ni Yesu Kristo pekee (MATHAYO 3:17; YOHANA 8:29). Ni kwa sababu hii, tunahesabiwa haki BURE kwa neema yake, kwa neema yake, kwa njia ya ukombozi ulio katika Kristo Yesu kwa imani katika damu yake iliyomwagika msalabani, alipokufa kwa niaba yetu, ili awe upatanisho (WARUMI 3:24-26; 1 TIMOTHEO 2:5-6).



(4) SABABU KUU YA KUMWITA MTUMISHI WA MUNGU KWAMBA ANA PEPO (MST.19-

20)

Mtumishi yeyote wa Mungu anayeyafichua maovu yaliyo……………………………. katika jamii ya watu wanaojiita Wakristo, na kuyanena waziwazi kwamba hayampendezi Mungu, na kuisema kweli, huyu sharti watu hao watamwita ana pepo. Dhambi zinapokubalika katika Kanisa lote la Mungu na watu wanaojiita Wakristo, wanapokuwa hawana tofauti na wapagani au mataifa, anapoinuliwa Mtumishi wa Mungu na kuleta mageuzi, sharti mtu huyo ataitwa ana pepo. Yesu hapa alifichua maovu yao na kuisema kweli kwamba wanataka kumuua, wao wakakana, wakaipinga kweli hiyo wakati ilikuwa kweli; kinyume chake wakamwita ANA PEPO, ili kujikosa na kuhalalisha maovu yao! (MST. 19-20, 23). Hivyo ndivyo inavyokuwa wakati awote. Haya yalimpata Martin Luther, John Wesley, Charles Finney na wote walioleta mageuzi ya jinsi hii nyakati zao.



(5) WAJIBU NA JINSI YA KUHUKUMU (MST. 21-24)

“Ifanyeni hukumu iliyo haki“, ni mafundisho ya Yesu Kristo kwetu. Hatupaswi kukaa kimya kwa visingizio vya Neno, “Msihukumu“, na kuacha kuyakosoa mafundisho potofu ya Mashahidi wa Yehova; Mormonism au Christ Church for Latter Day Saints, wanaoshika mafundisho ya Joseph Smith; au wanaojiita Wakristo na kusema wao siyo dhehebu, wanaofuata mafundisho ya William Branham; au mafundisho yanayofundisha watu kushika sabato leo, au mafundisho mengine yoyote yaliyo potofu. Kukaa kwetu kimya na kuogopa “kuyasema madhehebu mengine“, siyo kufuata nyayo za Mchungaji Mkuu wa Kondoo, Yesu Kristo na kufanya hivyo, ni kuwaachia kondoo wetu wararuliwe na mbwa mwitu. Huo ni uchungaji wa mshahara. Yesu aliifanya hukumu iliyo haki, pale alipokuwa kinyume na kuishika Sabato, na tena pale aliposema “Jilindeni na *chachu* au mafundisho ya Mafarisayo na Masadukayo“. (MATHAYO 16:11-12; YOHANA 10:12; MATENDO 20:28-30). Tunapaswa kufuata kielelezo cha Yesu. Kanisa la Kwanza walizingatia kufanya hivyo (WARUMI 16:17; 2 YOHANA 1:9-11). Watu wenye mafundisho potofu, hatupaswi kuwa na ushirika nao, tuwahesabu tu kama mataifa na kuwahubiria kweli na kutokukubali kusikia chochote kutoka kwao.



(1) SABABU KUU YA WATU WENGI KUSHINDWA KUMPENDEZA MUNGU

(MST.25-29)

Tangu zamani za kale, sababu kuu ya watu wengi kushindwa kumpendeza Mungu, ni watu hao kuacha kumwamini Yesu na kuokolewa, kwa kungoja kwanza WAKUU WAMWAMINI (MST. 26). Wengine wanangoja kwanza baba na mama, mume au kiongozi wao wa dini aokoke, ndiyo eti nao waokoke, na wanafuata mafundisho yao tu kimkumbo. Huu ni mtego mkubwa wa Ibilisi. Ukitengwa ugali mezani kila mtu huchukua tonge lake mwenyewe! Ndivyo ilivyo, damu imemwagika msalabani, wokovu tayari. Kila mmoja anapaswa kuuchukua kwa imani. Ni muhimu kukumbuka pia kwamba, kila mtu atalichukua furshi lake mwenyewe na kutoa habari zake MWENYEWE (WARUMI14:12; WAGALATIA 6:5). Hakuna haja ya kungoja wakuu waokoke ndiyo nasi tuokoke. Kufa hakufuati nani wa kwanza kuzaliwa!.



(7) SAA YA KUKAMATWA (MST. 20).

Maadui zetu watatutafuta sana ili watushike na kutudhuru, hata hivyo, hatupaswi kuhofu. Hatuwezi kufa mpaka saa yetu itakapowadia. Juhudi zao zitagonga mwamba, wakati wote Bwana wetu atatupa mlango wa kutokea maana amesema atakuwa pamoja nasi hat ukamilifu wa dahari yaani mwisho wa mambo yote (MATHAYO 28:19-20; AYUBU 5:20, 26-27).



(8) NAMI NILIPO NINYI HAMWEZI KUJA (MST. 33-36)

Hatuwezi kumwona Yesu pasipo Utakatifu na kutafuta kwa bidii kuwa na amani na watu wote (WAEBRANIA 12:14). Ni wale tu wenye mioyo safi watakaomwona Mungu (MATHAYO 5:8). Ikiwa tumejaa masengenyo, chuki, fitina, hasira, mawazo machafu, n.k. tutamtafuta Yesu tusimwone.

(9) MITO YA MAJI YALIYO HAI (MST. 37-44)

Mtu akimpokea Roho Mtakatifu, ishara ya kwanza itakayoonekana kwake, ni kunena kwa lugha mpya kadri roho atakavyomjalia kutamka (MATENDO 2:4; 10:44-46; 19:6). Maji yanapokuwa yanapita katika mto, hutoa aina fulani ya sauti isiyoweza kuelezeka. Ndivyo alivyo mtu anenaye kwa lugha baada ya kumpokea Roho, mito ya maji hutoka ndani yake!



(1) KOSA LA KUMHUKUMU MTU KABLA YA KUMSIKIA KWANZA NA KUJUA

ATENDAVYO (MST. 31-32, 45-52)

Watu wengi hufanya kosa la kumhukumu Mtumishi wa Mungu kabla ya kumsikia kwanza anenavyo au anavyofundisha na kujua atendavyo. Haitupasi kufanya hivi. Watumishi waliotumwa na makuhani kumkamata Yesu, walikubali kwanza kumsikia na wakagundua kweli waliyokuwa wamefichwa na Shetani. Kuna faida kubwa kuiga mfano wao.

…………………………………………………………………………………………………………………………………. .

Ni sifa ipi ya kutuwezesha kuingia mbinguni? Ni utakatifu (WAEBRANIA 12:14). Ndani yake hakitaingia kamwe chochote kilicho kinyonge (UFUNUO WA YOHANA 21:27). Kinyonge ni kipi? Ni yule anayetenda dhambi. Huyu ni mtu asiyefaa, ni mnyonge! Je, wewe ni mtakatifu? Jibu ni la! Maisha yako yamejaa dhambi, pamoja na kusema una dini; hivyo wewe pia ni mnyonge, hufai kuingia mbinguni. Ukitubu leo dhambi zako zote kwa kumaanisha kuziacha, na kuifuata njia ya Yesu Kristo, ndipo utakapopata rehema ya kuingia mbinguni (MITHALI 28:13; YOHANA 14:6). Je, uko tayari kutubu sasa ili upate rehema hii? Najua uko tayari. Basi fuatisha sala hii ya toba kwa dhati kutoka moyoni; “Mungu Baba asante kwa ujumbe huu. Hakika mimi ni mnyonge, mwenye dhambi. Sistahili kuingia mbinguni. Natubu dhambi zangu zote kwa kumaanisha kuziacha. Kuanzia leo nataka niifuate njia ya Yesu Kristo. Bwana Yesu niwezeshe. Asante kwa kunisikia katika Jina la Yesu. Amen”. Mpendwa msomaji umekubaliwa kuingia mbinguni. Ili uzidi kudumu katika utakatifu mpaka siku ya kuiaga dunia hii, hakikisha unahudhuria mafundisho katika Kanisa linalohubiri wokovu. MUNGU AKUBARIKI !!




Bwana ametupa neema tena siku hii ya leo, kuendelea kujifunza Kitabu cha YOHANA katika Biblia zetu. Leo, tutatafakari kwa makini YOHANA 8:48-59, na YOHANA 9:1-5. Kichwa cha somo letu la leo, “SABABU ZA KUUGUA“, ni moja tu kati ya vipengele vingi vya somo letu. Tutaligawa somo letu la leo katika vipengele saba:-

(1)KUVUNJIWA HESHIMA KWA MTUMISHI WA MUNGU (8:48-50);

(2)JINSI YA KUKWEPA MAUTI YA MILELE (8:51);

(3)YESU, MKUU KULIKO IBRAHIMU NA MANABII (8:52-58);

(4)KUJIFICHA KWA YESU (8:59);

(5)MTU KIPOFU TANGU KUZALIWA (9:1-3);

(6)SABABU ZA KUUGUA (9:3);

(7)KUZIFANYA KAZI ZA MUNGU MAADAMU NI MCHANA (9:4-5).



(1) KUVUNJIWA HESHIMA KWA MTUMISHI WA MUNGU (8:48-50)

Bwana wetu Yesu Kristo, hapa walimwita MSAMARIA, tena ANA PEPO. Wasamaria walikuwa ni maadui wakubwa wa Wayahudi na walikuwa hawachangamani kabisa (YOHANA 4:9). Wasamaria walihesabiwa kuwa ni WAASI (HOSEA 13:16), na Msamaria yeyote alipoonekana hekaluni Yerusalemu, walimpiga kwa “kipigo cha waasi“, na kumtoa nje ya hekalu. Wasamaria walikuwa washirikina sana na uchawi ulikuwa jadi yao (MATENDO 8:9-11). Hivyo basi, Mafarisayo na Waandishi, walipomwita Yesu, Msamaria; walikuwa na maana kwamba yeye ni adui wa taifa lao na dini yao, tena ni mchawi anayestahili kupigwa “kipigo cha waasi“, na kutolewa kati yao! Ilikuwa heri mtu alipoitwa MGALILAYA ambalo lilikuwa jina la kuwabeza watu walio dhaifu, wanyonge, wasio na kitu! (YOHANA 7:52; MARKO 14:70; LUKA 23:6). Mpaka leo, Wayahudi wanawaita Wakristo “CUTHAEI“, kwa kuwabeza. Jina “CUTHAEI“, lina maana ya WASAMARIA! Yesu hakuitwa tu Msamaria bali pia walimwita “ana pepo“ kwa maana kwamba ni mwendawazimu, na hivyo hakuna haja ya kuyasikiliza maneno yake (YOHANA 10:20). Mafarisayo hawa, pia walisema Yesu anatoa pepo kwa nguvu za mkuu wa pepo yaani shetani, hivyo walimwona ni Mtumishi wa Shetani na siyo Mtumishi wa Mungu! (MATHAYO 9:32-34). Ni muhimu kwetu kujifunza kwamba shetani atatumia watu wa namna zote hata Mafarisayo na Waandishi, yaani viongozi wa dini kuvunja heshima ya Watumishi wa Mungu wanaoihubiri kweli, ili watu wasiwasikilize. Paulo Mtume, aliitwa ana wazimu alipoisema kweli, (MATENDO 26:24-25). Hata manabii wa zamani pia waliitwa wana wazimu (2 WAFALME 9:1-11). Kanisa la Kwanza, kwa sababu lilihubiri kweli, LILINENWA VIBAYA KILA MAHALI(MATENDO 28:22). Hatupaswi kuona ajabu, Mtumwa si mkubwa kuliko Bwana wake. Yaliyompata Yesu, yatawapata Watumwa wake waaminifu leo (YOHANA 15:20-21). Tukidumu katika kweli lazima dhehebu letu litanenwa vibaya kila mahali, hizi ni kazi za kwaida za shetani nyakati zote! Yesu alisema, “Mimi sina pepo, lakini mimi namheshimu Baba yangu, na ninyi mwanivunjia heshima yangu“. Hapa hakujibu lolote juu ya yeye kuitwa Msamaria maana yeye ni MSAMARIA MWEMA! Pamoja na Yesu kuvunjiwa heshima hivyo, hakuitafuta heshima hiyo kwa nguvu kati yao! Heshima au utukufu wa kuutafuta mwenyewe, si utukufu (YOHANA 8:54; MITHALI 25:27). Yesu alimwachia Baba kutafuta utukufu wa kumpa, kati yao, na kuwahukumu yeye mwenyewe. Tunapovunjiwa heshima, tusijisumbue kuitafuta heshima hiyo kwa watu, kwa nguvu zetu. Tumwachie Mungu wetu kazihiyo, yeye huifanya vizuri sana kwa wakati wake, tunapodumu kuwa waaminifu kuitenda kazi yake. Vivyo hivyo ni muhimu kutambua kwamba wale wote wanaowaita Manabii wa Mungu kwamba ni wapumbavu, wana wazimu, wana pepo n.k; watapatilizwa au kuhukumiwa kwa maovu yao hayo (HOSEA 9:7).

(2) JINSI YA KUKWEPA MAUTI YA MILELE (8:51)

Jinsi pekee ya kukwepa mauti ya milele, ni KULISHIKA NENO la Mungu. Kulishika Neno ni tofauti na kulisikia. Kulishika Neno maana yake KULITENDA NENO (YAKOBO 1:22). Mtu anayelitenda neno la Mungu, hataopna mauti milele. Maana yake nini maneno haya? Je, mtu akiokoka na kudumu kulitenda Neno la Mungu, hatakufa kabisa? Jibu ni kwamba, watu waliookoka, WANAKUFA kama watu wengine (WARUMI 8:36; 2 WAKORINTHO 4:11; 2 WAFALME 13:14; 2 TIMOTHEO 4:6). Kinachosemwa hapa na Yesu, ni kwamba mtu anayelitenda Neno hataona MAUTI YA MILELE au MAUTI YA PILI yaani hatatupwa katika ziwa la moto (UFUNUO 20:6; 21:8). Kufa kwa mtu anayelitenda Neno ni kupita katika mlango wa uzima na kwenda kukaa pamoja na Bwana Yesu (2 WAKORINTHO 5:6,8).



(3) YESU, MKUU KULIKO IBRAHIMU NA MANABII (8:52-58)

Ibrahimu alikufa, manabii wote walikufa, na makaburi yao yako hata leo. Yesu aliye mkuu kuliko hao, Yeye alikufa na kufufuka siku ya tatu kama alivyosema. Kaburi lake, liko wazi hivi leo (MATENDO 2:29-36; LUKA 24:3). Yesu Kristo alikuwako tangu zamani za kale, tangu milele, kabla ya Ibrahimu, kabla ya vitu vyote (MIKA 5:2; WAKOLOSAI 1:17). YESU NI MUNGU(1 YOHANA 5:20; TITO 2:13), hivyo hana baba, hana mama, hana wazazi, hana mwanzo wala mwisho wa siku zake (WAEBRANIA 7:3). Yesu hakuanza kuwapo alipozaliwa na Mariamu. Katika MST. 54, Yesu anasema “Anitukuzaye ni Baba yangu ambaye ninyi mwanena kuwa ni Mungu wenu“. Watu hawa WALINENA TU kuwa ni Mungu wao, lakini ukweli hawakumjua Mungu (1 YOHANA 2:3-5).



(4) KUJIFICHA KWA YESU (8:59)

“Wakaokota mawe ili wamtupie“. Waliokota mawe haya ili wamtupie, kwa sababu alionekana kwao kwamba ANAKUFURU, kwa kusema kabla Ibrahimu hajakuwako, yeye alikuwako, na kwamba Ibrahimu alishangilia kuiona siku ya kuwako Yesu duniani. Kwa kuwaza hivyo, waliichukua sheria ya MAMBO YA WALAWI 24:16 mikononi mwao. Yesu alijificha, akatoka hekaluni. Hapa tunajifunza juambo la msingi. Hatupaswi kuwaacha watu watuonee wakati tuna uwezo wa kujificha au kukimbia, kwa visingizio vya kukubali kuteswa kwa ajili ya Kristo. Uzima wetu ni wa thamani sana kwa ajili ya Injili. Mume ambaye hajaokoka anapotupiga na kutaka kutuua, hatuna budi kujificha na kutoka nje!



(5) MTU KIPOFU TANGU KUZALIWA (9:1-3)

Baada ya Yesu kuvunjiwa heshima kiasi hicho, hakuacha kutenda kazi ya Mungu au kubadili msimamo wake! Aliendelea kuitenda kazi ya Mungu kwa msimamo wake uleule! Hii ndiyo siri ya kutumiwa sana na Mungu! Vilevile wanafunzi wake hawakumwacha na kuona aibu kuambatana na Mchungaji wao, aliyenenwa vibaya na kuitwa ANA PEPO! Ssisi nasi tunapaswa kufuata mfano wa wanafunzi hawa. Kamwe tusione aibu kuambatana popote na Mchungaji anayesemwa vibaya kila mahali, na kuambiwa ana pepo au yeye ni pepo, wakati tuna hakika kwamba anafundisha kweli. Hapa Yesu anakutana na mtu kipofu tangu kuzaliwa na kutufundisha kwamba sisi sote ni vipofu tangu kuzaliwa kwetu kutokana na dhambi zetu. Kipofu hutembea gizani na kuanguka shimoni pasipo kupenda. Ndivyo alivyo mwenye dhambi yeyote. Mtu akikataa kwamba yeye siyo kipofu hawezi kusamehewa dhambvi zake (YOHANA 9:39-41; ZABURI 51:5; WARUMI 3:23; 1 YOHANA 1:8-10).



(6) SABABU ZA KUUGUA (9:3)

Wako watu wengine waliookoka ambao wakiona wake zao, waume zao au wapendwa wengine wanaugua, huwaambia kwamba wanaugua kwa sababu wametenda dhambi. Huku ni kuitia jeraha dhamiri iliyo dhaifu na kumtenda dhambi Kristo (1 WAKORINTHO 8:11-12). Hatupaswi kuhukumu hivyo. Ziko sababu nyingi zinazoweza kumfanya mtu awe mgonjwa:-
Dhambi (ZABURI 38:3-4; YEREMIA 30:12-14; YOHANA 5:14);
Ili Mungu ajipatie utukufu kwa kumponya kwa muujiza (YOHANA 11:1-4);
Ili kazi za Mungu zidhihirishwe ndani ya mtu huyo (YOHANA 9:3);
Kutokana na KUONEWA na Ibilisi (MATENDO 10:38);
Kumpa Ibilisi nafasi kwa kushindwa kumpinga na kumkemea (WAEFESO 4:27; YAKOBO 4:7);
Upungufu wa Imani (MATHAYO 17:18-20; MARKO 6:5-6).

Ikiwa hatujatenda dhambi yoyote, hatupaswi kudanganywa na Ibilisi kwamba ugonjwa uliotupata umetupata sababu ya dhambi. Zakaria na Elisabeti walikuwa tasa, lakini walikuwa wenye haki mbele za Mungu bila lawama yoyote (LUKA 1:5-7). Tukimruhusu Shetani atudanganye hivyo, mioyo yetu hutuhukumu bure na kutukosesha ujasiri kwa Mungu, na hivyo maombi yetu huwa hayapati majibu (1 YOHANA 3:21-22).



(7) KUZIFANYA KAZI ZA MUNGU MAADAMU NI MCHANA (9:4-5)

Giza linakuja, na wakati wa kulala utafika. Kama baba zetu walivyolala, sisi nasi tutalala au kwa maneno mengine, tutakufa. Siku ya kufa hatuijui. Tufanye kazi ya Mungu kana kwambaKESHO HAIKO. Hii ndiyo siri ya kufanikiwa.



…………………………………………………………………………………………………………………………………. .

Ni sifa ipi ya kutuwezesha kuingia mbinguni? Ni utakatifu (WAEBRANIA 12:14). Ndani yake hakitaingia kamwe chochote kilicho kinyonge (UFUNUO WA YOHANA 21:27). Kinyonge ni kipi? Ni yule anayetenda dhambi. Huyu ni mtu asiyefaa, ni mnyonge! Je, wewe ni mtakatifu? Jibu ni la! Maisha yako yamejaa dhambi, pamoja na kusema una dini; hivyo wewe pia ni mnyonge, hufai kuingia mbinguni. Ukitubu leo dhambi zako zote kwa kumaanisha kuziacha, na kuifuata njia ya Yesu Kristo, ndipo utakapopata rehema ya kuingia mbinguni (MITHALI 28:13; YOHANA 14:6). Je, uko tayari kutubu sasa ili upate rehema hii? Najua uko tayari. Basi fuatisha sala hii ya toba kwa dhati kutoka moyoni; “Mungu Baba asante kwa ujumbe huu. Hakika mimi ni mnyonge, mwenye dhambi. Sistahili kuingia mbinguni. Natubu dhambi zangu zote kwa kumaanisha kuziacha. Kuanzia leo nataka niifuate njia ya Yesu Kristo. Bwana Yesu niwezeshe. Asante kwa kunisikia katika Jina la Yesu. Amen”. Mpendwa msomaji umekubaliwa kuingia mbinguni. Ili uzidi kudumu katika utakatifu mpaka siku ya kuiaga dunia hii, hakikisha unahudhuria mafundisho katika Kanisa linalohubiri wokovu. MUNGU AKUBARIKI !!!

0 comments:

Post a Comment

 
Blogger Templates